Mwanamuziki mashuhuri wa nchini Marekani Whitney Houston ameaga
dunia. Polisi mjini Los Angeles wamesema Whitney ambaye alikuwa na umri
wa miaka 48, amekutwa amekufa katika hoteli iliyopo mtaa wa Beverly
Hills.
Habari za kifo cha nyota huyo zimekuja wakati ulimwengu wa muziki
ukijiandaa kwa sherehe za tuzo ya Grammy leo Jumapili, na pia saa chache
kabla ya tafrija ya chakula kwenye hotel ambapo marehemu Whitney
Houston amepatwa na mauti.
Afisa wake wa habari Kristen Foster ambaye alikuwa wa kwanza kutangaza
kifo hicho hakuelezea chanzo cha kifo chake. Hata hivyo katika miaka ya
hivi Karibuni mwanamuziki huyo amekuwa akisumbuliwa na athari za
matumizi ya madawa ya kulevya.
Muziki wa Whitney Houston aliuza albamu zaidi ya milioni 170
Whitney Houston alijipatia Umaarufu mkubwa katika miaka ya 1980 na
1990, kwa nyimbo zilizovuma kama ''How will I Know'', ''Saving all my
Love for You'' na ''I will always Love You''. Alishiriki pia katika
uwanja wa uigizaji na kuwa katika filamu mashuhuri ya ''Bodyguard''
Wakati wa umaarufu wake Whitney Houston alishinda tuzo sita za Grammy.
Magwiji wa muziki wametoa rambi rambi zao kupitia mitandao ya kijamii,
wakimueleza Bi Houston kama mtu ambaye hatasahaulika katika fani ya
Muziki.
No comments:
Post a Comment