Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Kiongozi wa
Upinzani Bungeni, Mheshimiwa Freeman Mbowe, kuomboleza kifo cha Mbunge
wa Viti Maalum wa chama hicho, Mheshimiwa Regina Mtema.
Mheshimiwa Mtema ambaye pia alikuwa Mjumbe
wa Kamati Kuu ya Chadema na Waziri Kivuli wa Kazi na Ajira amefariki
dunia katika ajali ya gari iliyotokea maeneo ya Ruvu, Mkoa wa Pwani,
asubuhi ya leo Jumamosi, Januari 14, 2012.
Katika salamu zake, Mheshimiwa Rais
Kikwete amemwambia Mheshimiwa Mbowe kuwa amesikitishwa na kuhuzunishwa
na habari za kifo cha mbunge huyo ambaye amepoteza maisha akiwa bado
kijana na kwamba pigo hilo siyo kwa Chama cha Chadema peke yake bali ni
kwa taifa zima.
“Nimepokea kwa masikitiko na huzuni nyingi
habari za kifo cha Mheshimiwa Mtema katika ajali ya gari. Siyo kwamba
ajali hii imechukua maisha ya kijana bali imelinyang’anya taifa mbunge
hodari, na kwa hakika, kifo chake siyo tu ni pigo kwa chama chako cha
CHADEMA bali ni pigo kwa sote na kwa taifa letu kwa jumla. Nakutumia
wewe binafsi, chama chako na wanachama wake salamu za dhati ya moyo
wangu kuomboleza kifo na msiba huu mkubwa.”
“Napenda ujue kuwa niko nanyi katika msiba
huu. Napenda vile vile uniwasilishie salamu zangu za rambirambi za
dhati kabisa kwa wana-familia, ndugu na jamaa wa marehemu Mheshimiwa
Mtema. Wajulishe kuwa nimepokea habari hizo kwa uchungu mwingi na kuwa
moyo wangu uko nao katika wakati huu mgumu wa maombolezo, “ amesema
Mheshimiwa Rais na kuongeza.
“Aidha, wajulishe kuwa nawaombea kwa
Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, awajalie uvumilivu na subira katika
kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi yake. Naungana nawe,
Mheshimiwa Mwenyekiti, na wanafamilia wa marehemu kumwomba Mwenyezi
Mungu aiweke pema peponi roho ya Mheshimiwa Regina Mtema. Amen.”
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu,
DAR ES SALAAM.
14 Januari, 2012
No comments:
Post a Comment