Monday, December 26, 2011

KIFO CHA KHALIL IBRAHIM CHAZUA WASIWASI JIMBO LA DARFUR

  DW

Kundi kuu la waasi katika jimbo la Darfur, The Justice and Equality Movement – JEM- limethibitisha kuwa kiongozi wake aliuwawa na wanajeshi wa Sudan na likaapa kulipiza kisasi


Wakati jeshi la Sudan likisema kiongozi huyo wa waasi, Khalil Ibrahim, aliuwawa katika mapambano akijaribu kuingia kisiri hadi Sudan Kusini wiki iliyopita, kundi la waasi la JEM lilipinga, likisema aliuwawa katika shambulizi la angani, na kudai nchi za magharibi zilihusika katika shambulizi hilo.
Gazeti la Sudan Tribune lilinukuu taarifa ya kundi la JEM iliyosema tukio hilo linaashiria ushirikiano na njama ya baadhi ya nchi za eneo hilo na kimataifa na serikali ya mauaji ya kimbari katika jimbo la Darfur.

Kulingana na msemaji wa kundi hilo, ambalo lilijiondoa kitoka mpango wa amani na serikali mwaka jana, amesema kwa kufanya njama hiyo, serikali ya Sudan imefungua milango ya mauaji ya kisiasa.

Ibrahim yadaiwa alirejea kutoka nchini Libya mwaka huu, baada ya kuanguka kwa utawala wa Muammar Gaddafi, ambapo kundi la JEM lilipata msaada. Taifa jipya huru la Sudan Kusini pia linashtumiwa na serikali ya Sudan kwa kuwasaidia waasi.

Kulingana na ripoti na mikanda ya video inayoenezwa kwenye mitandao ya internet, polisi mjini Khartoum waliwatawanya wafuasi wa JEM waliojaribu kutoa rambirambi zao nyumbani kwa familia ya Ibrahim viungani mwa mji huo mkuu wa Sudan. Haijabainika ni nani atakayechukua mahala pa kiongozi wa kundi hilo la waasi ambalo aliliunda mwaka 2000.

#b#Katika mzozo wa Darfur, ambao umeendelea tangu mwaka 2003, zaidi ya watu laki tatu wameuwawa kulingana na Umoja wa mataifa, ijapokuwa serikali ya Sudan inasema idadi hiyo iko chini.

Waziri wa habari wa Sudan, Abdullah Massar, amesema kifo cha Ibrahim kinatuma ujumbe kwa makundi ya waasi kuisikia sauti ya busara na kujiunga na mchakati wa kutafuta amani. Alisema jana kuwa milango yao iko wazi na kwamba mkataba wa Doha ungali wazi.

Kifo cha Ibrahim, ambaye kila mara alitajwa kuwa kiongozi jasiri, huenda kikawa pigo kubwa kwa kundi la waasi wa JEM. Mtalaamu mkuu nchini Sudan, Alex de Waal, amesema Khalil Ibrahim alitawala kundi la JEM na kibinafsi alibaini mikakati ya kisiasa na kijeshi ya kundi hilo na hasa ndiye aliyezuia kundi hilo kufanya mazungumzo ya amani na serikali ya Sudan, hivyo kifo chake ni pigo kubwa kwa waasi hao.

Uongozi katika mji mkuu wa Khartoum utahisi kukichukulia kifo chake kwa kuzingatia kuwa uasi katika jimbo la Darfur sasa umekwisha. Wakati tishio linalotolewa na kundi la JEM bila shaka likionekana kupungua, inaweza kuwa makosa kwa serikali kudhani kuwa mgogoro wa kisiasa katika jimbo la Darfur unaweza kutatuliwa kwa urahisi.

No comments:

Post a Comment